Saturday 13 August 2016

Kilimo cha Mbaazi


Mbaazi ni zao jamii ya mikunde inayostawi katika nchi za kitropiki zenye mvua chache. Zao hili ni muhimu sana kwa nchi za Asia ambako ni mojawapo ya chakula kikuu hasa katika nchi ya India.

Kwa miaka ya hivi karibuni, zao la mbaazi limekuwa moja ya mazao muhimu ya biashara katika maeneo mengi ulimwenguni. Hii ni kutokana na ongezeko la walaji na uwezo wake wa kustahimili ukame na mvua chache ambao unaendana na mabadiliko ya hali ya hewa ulimwenguni kote. Nchini Tanzania, zao hili hulimwa kwa wingi katika mikoa ya Manyara (Hanang na Mbulu), Arusha (Arusha vijijini na Meru), Dodoma (Kondoa), Kilimanjaro (Same, Mwanga, Rombo, Hai na Moshi vijijini) Mbaazi kwa kawaida hupandwa kwa msimu mmoja lakini aina za kienyeji zinaweza kulimwa kama zao la kudumu ambapo huweza kukaa shambani miaka mitatu hadi mitano ingawa uzalishaji wa mazao hupungua msimu hadi msimu.



Matumizi ya Mbaazi
Chakula/mboga hasa zikiwa mbichi. Mbaazi mbichi huwa na protini zaidi ya asilimia 21%, wanga asilimia 44.8%, mafuta asilimia 2.3% pamoja na baadhi ya virutubisho vya madini kama chokaa na chuma.
Zao la biashara. Kutokana na kuwepo kwa aina bora za mbaazi zinazohitajika kwa wingi katika soko la ndani na nje pamoja na kuwepo kwa aina zinazokomaa mapema na kuwahi soko la dunia, zao hili limekuwa likilimwa kwa ajili ya biashara hasa katika wilaya za Babati, Karatu, Arumeru pamoja na Kondoa
Chanzo cha nishati (kuni). Miti ya mbaazi hutumiwa kwa ajili ya kuni katika maeneo ya ukanda wa chini ambayo haina miti. Matumizi haya pia husaidia kupunguza uharibifu wa mazingira kutokana na watu kutokukata miti ovyo.
Kirutubisho cha udongo. Mbaazi ni jamii ya mikunde ambayo huongeza mbolea aina ya Naitrojeni kwenye udongo. Majani yake yanapopukutika na kudondoka ardhini huoza na kubadilika kuwa mbolea ambayo pia huboresha muundo wa udongo. Chakula cha mifugo. Maganda na majani ya mbaazi hutumika kama chakula kwa ajili ya kulishia mifugo.
Hali ya hewa
Mbaazi hustawi vizuri katika nyuzi joto 29 hadi 38, na hupandwa kuanzia usawa wa bahari hadi mita 1900 kutegemeana na aina ya mbegu. Kuna mbegu zinazostawi katika ukanda wa chini, wa kati na wa juu. Aidha kuna aina zinazostawi zaidi ya mita 2000 kutoka usawa wa bahari Zao hili huhitaji kiasi cha milimita 600 hadi 1000 cha mvua kwa mwaka. Aina za mbaazi za muda mfupi hutosha kustawi katika mvua kiasi cha milimita 250 hadi 370 kwa mwaka.
Udongo
Kwa kilimo chenye tija, ni vizuri kuotesha mbaazi kwenye udongo unaoruhusu maji, wenye mbolea kiasi na wenye tindikali kiasi cha pH kuanzia 5 hadi 7.



UTAYARISHAJI WA SHAMBA.
• Shamba la mbaazi litayarishwe mapema kwa kung’oa mabaki yote ya mimea pamoja visiki kabla ya kulilima.
• Lima shamba kiasi kisichopungua sentimeta 30.
• Lainisha udongo kwa kupitisha haro.
• Tayarisha matuta au makinga maji kama shamba liko kwenye mteremko.
Kuandaa mbegu
• Mbegu bora iliyochaguliwa vizuri na kuhakikiwa kiwango cha uotaji ziandaliwe.
• Mbegu ziwekewe dawa ya kuzuia kuvu (fungus) kabla ya kupanda ili kuzuia magonjwa yatokanayo na mbegu na udongo.
 Mbegu bora
Mbegu za mbaazi zimegawanyika katika makundi makubwa matatu nazo ni, mbegu za muda mfupi, mbegu za muda wa kati, mbegu za muda mrefu.

KUPANDA.
 1. Mbaazi za muda mfupi, zipandwe peke yake bila kuchanganya na mazao mengine. Nafasi: Kuwe na nafasi ya sentimeta 75 toka mstari na mstari, sentimita 20 toka shimo hadi shimo. Kiasi cha mbegu: Kilo 5 hadi 6 zaweza kutumika kwa ekari moja.

 2. Mbaazi za muda wa kati, zipandwe peke yake na katika mwinuko kutoka usawa wa bahari wa mita 1000 hadi 1880 Nafasi: Kuwe na nafasi ya sentimita 120 toka mstari hadi mstari na sentimita 30 toka shimo hadi shimo. Kiasi cha mbegu: Waweza kutumia kilo 5 kwa ekari moja.

3. Mbaazi za muda mrefu, zipandwe peke yake katika mwinuko toka usawa wa bahari wa mita 1000 hadi 1880. Nafasi: Kuwe na sentimita 150 toka mstari hadi mstari na sentimita 50 toka shimo hadi shimo. Kiasi cha mbegu: Waweza kutumia kilo 5 kwa ekari moja

PALIZI NA KUPUNGUZIA MIMEA.
Ni muhimu kupalilia mapema (angalau mara mbili kulingana na kiasi cha unyevu au mvua) na kuondoa magugu ambayo hushindana na mimea michanga. Miche ikiwa mingi kwenye shina husababisha mazao kuoza. Kwa hivyo ni muhimu kupunguza miche na kubaki miwili au kutegemeana na nafasi.

 WADUDU.
Kuna wadudu wa aina mbalimbali ambao kushambulia mbaazi, wakati zikiwa shambani au zikiwa galani.
1.       Vidukari
 Vidukari weusi wanaotembea kwa makundi na ambao huonekana zaidi katika sehemu changa za mimea kama vichomozo, matawi na majani. Wadudu hawa husambaa kwa wingi wakati wa majira ya ukame. Wadudu hawa hufyonza majimaji au utomvu ulio kwenye maeneo hayo na kusababisha mbaazi kubadilika rangi na kukauka. Udhibiti….Wadudu hawa hudhibitiwa kwa kutumia njia bora za kilimo na kufanya kilimo cha mzunguko.

2.       Kunguni wa mifuko ya mbaazi
 Kuna aina nne za wadudu hawa ambao ni Kunguni wa kahawia (Claiigralla spp), Kunguni wakubwa (Anoploenemies spp), Riptutasi (Riptortus dentipes), Kunguni wa kijani (Nezara viridula). Wadudu hawa hufyonza mbegu inayokuwa kupitia kuta za mifuko na kufanya mbegu kuoza na kukosa thamani ya kuwa mbegu na chakula cha binadamu. Udhibiti….Wadudu wanaofyonza mifuko ni vigumu kuwadhibiti kwani huruka kutoka sehemu moja na kwenda nyingine hivyo wanaweza kukusanywa kwa chandarua na kuangamizwa.

3.       Mbawakavu wa maua na chavua (Blister beetles)
 Wadudu hawa wenye rangi ya njano hula maua na kupunguza uzalishaji wa mifuko ya mbaazi. Katika eneo ambalo uzalishaji wa mbaazi ni mkubwa, wadudu hawa hufanya uharibifu mdogo kuliko katika eneo ambalo mbaazi huzalishwa kwa kiasi kidogo. Udhibiti….Wadudu hawa wanaweza kudhibitiwa kwa kuwaondoa kwa mikono na kuwauwa isipokuwa wakati wa kuwashika kuwepo na uangalifu kwani wakisumbuliwa huweza kutoa kemikali ambayo inaweza kuunguza mikono au mwili.

4.       Funza wa vitumba (Maruca vitrata)
Wadudu hawa hutaga mayai kwenye vikonyo vya mbaazi kabla ya kuchanua au juu ya mifuko hula vikonyo vya maua na mbegu iliyoko ndani ya mifuko ya mbaazi. Udhibiti….Mkulima anaweza kuwadhibiti wadudu hawa kwa kufanya ukaguzi wa shamba mara kwa mara ili kufahamu uwepo wa wadudu hawa, pamoja na kutumia viuatilifu kulingana na maelekezo ya mtaalamu wa kilimo. Ni vyema ukaguzi ukafanyika wiki moja kabla ya mbaazi kuchanua na baada.

5.       Inzi wa mifuko (Melanagromyza chacosoma)
Hawa ni wadudu wadogo weusi warukao na wanaotaga mayai katika kuta za mifuko za mbaazi inavyokua. Funza wake ni weupe na wana urefu wa sentimeta 3. Wadudu hawa hufanya uharibifu mkubwa kwa kula mbegu changa iliyopo kwenye mifuko. Udhibiti….Katika maeneo ambayo wadudu warukao ni tatizo, jamii ya mikunde inayokomaa kwa muda tofauti isipandwe kwenye shamba moja ili kuzuia mwendelezo wa kuzaliwa kwa inzi hawa hasa kila aina ya mikunde inapotoa maua. Pia mwarobaini waweza kunyunyiziwa mara 4 kila baada ya wiki kwa kiwango cha gramu 50.

6.       Vithiripi (Megalurothrips spp. And Frankliniella schultzei)
Wadudu hawa wadogo na wenye rangi ya kahawia na mabawa ya njano huathiri mbaazi hasa kwa kufyonza utomvu kwenye majani na maua.Husababisha maua na vikonyo kusinyaa, kufifia rangi na kudondoka kabla ya kukomaa. Udhibiti….Kagua shamba kila mara ili kufahamu uwepo wa wadudu hao kabla ya mimea kuchanua ili kudhibiti mapema.

7.        Vipekeche
 Hawa ni wadudu wanaoshambulia mbaazi ikiwa ghalani. Wadudu hawa hutoboa mbegu na kutengeneza mashimo ya kutokea wadudu kamili.

No comments:

Post a Comment